NHK WORLD > Jifunze Kijapani > Mwanzo wa ukurasa wa Kiswahili > Mwalimu Tufundishe > Kauli ya heshima (Somo la 38)

Mwalimu Tufundishe

Kauli ya heshima (Somo la 38)

Unatumia kauli ya heshima unapozungumza na, au unapomtaja mtu aliyekuzidi umri, kiongozi wako, mwalimu, wateja, au mtu ambaye humfahamu vizuri.
Hata kwa watu ulio na mazoea ya kuzungumza nao kwa namna ya kawaida, unatumia maneno ya heshima unapozungumza nao katika matukio yaliyo rasmi kama vile mikutano ya kibiashara. Kilicho muhimu ni mazingira ya pale unapozungumzia.

Kuna aina mbili za vitenzi vinavyoashiria heshima.
Moja wapo ni “maneno ya staha.” Ikiwa unatumia maneno ya staha kuelezea vitendo au hali ya mtu unayezungumza naye au unayemzungumzia, unaweza kuonyesha heshima kwa mtu huyo.
Kwa mfano, “neno la staha” la MIMASU, (kuona/ kutazama), ni GORAN NI NARIMASU. Aina nyingine ni “maneno ya kunyenyekea.” Unayatumia, ikiwa unazungumzia vitendo au hali yako. Dereva wa teksi aliyeangaziwa katika mazungumzo ya leo, alipotaka kusema “Sawa / Nimeelewa,” hakusema WAKARIMASHITA. Badala yake alisema KASHIKOMARIMASHITA, ambalo ni neno la kunyenyekea linalomaanisha “nimeelewa.”
Unaweza kufikiria ni vigumu kutumia maneno ya heshima. Usiwe na wasiwasi. Katika mazungumzo ya kawaida, ikiwa utatumia vitenzi vya umbo la MASU, unaweza kusikika kiungwana tayari.
*Utatoka kwenye tovuti ya NHK.